E-mail from Anonymous Feb.1(in Swahili)


Wed, 31 Jan 1996 08:14:47 +0300 (EAT)
Assalaam alaykum,
1. Mgomo wa wanafunzi Pemba bado unaendelea. Inakisiwa kama asilimia 70 ya wanafunzi wanaendelea kugoma. Mapuri anasema SMZ itazifunga skuli zinazogoma. Amesema kuwa wanafunzi wanaogoma hawatachukuliwa hatua ila wale wanaowashawishi kugoma ndio watachukuliwa hatua. Pemba kuna wanafunzi kama 60,000 kati ya wanafunzi 150,000 wa Zanzibar nzima.

2. Wawakilishi wa CUF hawakuhudhuria semina ya Baraza la Wawakilishi kwa siku ya pili. Bado Mwakilishi Mohamed Mula hajaachiwa. Ahmed Seif yeye aliachiwa kwa dhamana ya Sh. 50,000. Wamesema hawahudhurii mpaka mwenzao atakapoachiwa. Semina hiyo inamalizika leo. Katika semina hiyo, katibu Mkuu, Wizara ya Katiba na Sheria, Othman Masoud, jana alitahadharisha kuwa haki na kinga za wawakilishi zilizoainishwa katika Katiba zinahitaji uangalifu kuzitumia.

3. Mbunge mmoja wa NCCR (Musoma vijijini), Paul Ndobho, amesema kuwa Mkapa asikwepe jukumu lake la kuhakikisha kuwa Pemba kuna usalama. Amesema kuwa Ulinzi na Usalama ni sehemu ya mambo ya Muungano yanayomhusu Mkapa. Aliyasema hayo kwenye semina ya Bunge inayoendelea hapa Dar. Mbunge Ali Moh'd Shela (Kiwani) alishangaa kuwa serikali ya Mkapa inasema inashughulikia masuala ya rushwa na wasiolipa kodi lakini mpaka leo hakuna mla rushwa mkubwa hata mmoja au anayekwepa kodi aliyeshikwa. Bunge la vyama vingi kwa kweli linasisimua.

Mbunge Sanya (Mkunazini) alichekesha wabunge aliposema alikuwa akipongezana na mwanafunzi wake wa kike kichochoroni alipomuona askari polisi akiwa na sare zake za kiaskari huku akiwa amevaa kanda mbili (ndara). Kilichowachekesha watu ni huko kupongezana kichochoroni ingawa baadaye aliwatoa wasiwasi wenzake kuwa hakuwa akifanya lolote baya na mwanafunzi wake huyo. Mbunge Sanya alikuwa anakusudia kuwatetea askari polisi ili hali zao ziwe nzuri.

Fatma Maghimbi (CUF, Chake) ameshangaa kuona kuwa nafasi za uwaziri kwa wanawake zinazidi kupungua. Awamu ya 2 kulikuwa na mawaziri wanawake wanne lakini sasa ni watatu tu. Alisema hiyo ni ishara kuwa 2000 kutakuwa na wawili tu kama trend hiyo itaendelea.

Ndugu Philip Marmo (Mbulu) kachaguliwa Naibu Spika wa Bunge.

4. Walioshikwa na Majira Unguja wamehukumiwa kulipa faini ya Sh 30,000 au jela mwaka mmoja. Mbarouk Yusuf na Yohana Stanley ndio wamehukumiwa hivyo. Wote wamelipa faini.

Samahani nimo harakani.
Tue, 30 Jan 1996 12:16:40 +0300 (EAT)
Assalaam alaykum,
Naona dhiki kubwa kuwa kila siku nawaelezea taarifa mbaya tu za kuhusu nchini kwetu. Lakini kwa kweli hivyo ndivyo mambo yalivyo. Jana nilikuwa nikisikiliza taarifa ya habari ya saa moja za usiku ya Sauti ya Tanzania Zanzibar na hakuna hata habari moja iliyokuwa nzuri: yote yalikuwa ni mambo ya siasa tena sio ya kufurahisha.

1. Watu watatu wamekamatwa Wete, Pemba kwa tuhuma za kutaka kulitia moto jengo la Baraza la Wawakilishi lilioko mjini hapo. Watu hawa walikamatwa na polisi baada ya kwisha kutupa bomu la petroli kwenye jengo hilo na wakiwa na madebe mengine ya petroli. Moto uliwahiwa na ukazimwa kabla ya kuleta madhara makubwa. Majina ya waliokamatwa hayakutolewa.

2. Waziri Mkuu, Sumaye amesema malumbano kuhusu Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar yamalizwe kwani hayamsaidii chochote mwananchi wa kawaida. Aliyasema hayo kwenye ufunguzi wa semina ya siku 3 ya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi. Wawakalishi wote wa CUF wameisusia semina hiyo kupinga kukamatwa juzi kwa wawakilishi wenzao wawili, Ahmed Seif (Utaani) na Mohamed salim Ali (Mkoani), huko Pemba.

3. Mbarouk Yusuf Khamis alifikishwa mahakamani jana kujibu shtaka la kukamatwa na nakala ya gazeti la Majira la tarehe 27 Jan., bandarini Unguja akitokea Dar es Salaam.

4. Rais Mkapa ameziomba nchi wahisani kusaidia kuelimisha kuhusu utamaduni wa vyama vingi ili wananchi waweze kuheshimu sheria na serikali ya chama kilichoshinda. Aliyasema hayo kwenye mazungumzo yake na Bibi Lynda Chalker, Waziri wa maendeleo ya nchi za nje wa Uiengereza katika ziara yake ya siku tatu nchini. Akizungumzia Zanzibar, aliwataka wahisani kuwaeleimisha wapinzani ukweli kwamba ni kinyume cha sheria na maendeleo ya demokrasia kwa chama kilichoshindwa kuleta vurugu badala ya kuwa mshiriki katika maendeleo na serikali iliyopo madarakani. (Maoni yangu: Huyu ni ngariba wa Kilwa - akata wenziwe kumbe yeye yu vivyo!! Maneno hayo yalikuwa yaelekezwe kwa CCM kwanza).

5. Dr. Omar Ali Juma, Makamu wa rais, amewataka wanasiasa nchini na nje ya nchi kuacha kuchochea uasi dhidi ya serikali ya Zanzibar na kuutaka upinzani kuitambua serikali hiyo ili kuwepo mazungumzo yatakayoleta suluhu, taarifa ya kutoka ofisi ya Makamu wa Rais imeeleza. Aliyasema hayo kwenye mazungumzo na Balozi wa Denmark nchini, Bw. Flemming Pederson. Dr. Omar alilalama kuwa wahisani wanawasikiliza zaidi upande wa upinzani kuliko upande wa serikali hivyo kufanya mvutano uendelee.

6. Mbunge Elizabeth Kasembe (Wanawake- CUF) atampeleka mahakamani Mbunge, haji Juma Haji (CCM- Matemwe) kwa madai ya kumdhalilisha kijinsia. Mbunge Elizabeth anadai kuwa Mbunge Haji alimwambia yeye (Elizabeth) ni 'bibi wa wakubwa' ndio maana akachaguliwa kuwa Mbunge. Kwa ushauri wa Spika Msekwa, na kwa kuwa tukio hilo lilitokea nje ya Bunge, Mbunge Elizabeth anakusudia kuchukua hatua za kisheria kwa mujibu wa sheria za Tanzania na sio kanuni za Bunge. Tayari ameshamuona wakili Richard Rweyongoza kufungua mashitaka.

7. Mgomo wa wanafunzi Pemba ulianza jana kwa wanafunzi kadhaa kutohudhuria skuli ingawa wapo waliohudhuria kama kawaida. Wilaya ya Wete na Mkoani ndizo zilizoongoza kwa mahudhurio mabaya. Kaimu Afisa Mdhamini wa Wizara ya Elimu Pemba, Uledi Juma Wadi alisema kuwa mgomo huo ulizikumba zaidi skuli za Jadida, Miti Ulaya, Kizimbani na Utaani zote za Wete, Pemba. Kwa mfano Utaani yenye wanafunzi 563, 407 hawakuhudhuria.

Mahudhurio pia yalikuwa mabaya kwa shule ya sekondari ya ufundi ya Kengeja, skuli ya Mwambe na Ngwachani. Shamiani, Fidel Castro na Chanjamjawiri hazikuathiriwa na mgomo huo wakati Ziwani na shule nyengine za Chake Chake ziliathiriwa kiasi. Mgomo huo haufahamiki utaendelea kwa siku ngapi.

Ah, yanatosha kwa leo!
Mon, 29 Jan 1996 13:27:46 +0300 (EAT)
Assalaam alaykum,
SMZ imemuweka ndani Mwakilishi wa Jimbo la Utaani, Wete, Pemba, kwa tiketi ya CUF, Bw. Ahmed Seif Hamad. Alikamatwa juzi akitoka msikitini kuswali Isha na Taraweikh. Mwakilishi mwengine wa Jimbo la Mkoani (wa CUF), Bw. Mohamed Mula anasakwa na polisi.

Wote wawili wanashutumiwa kuhusika na kuchochea mgomo wa wanafunzi wa Pemba nzima, uliopangwa kuanza leo, Jumatatu, kupinga uamuzi wa SMZ uliofanywa juu ya baadhi ya wanafunzi wa Karume Technical College (KTC) wanaotoka Pemba. Inasemekana kuwa wawakilishi hao walihutubia mikutano ya kuwashawishi wazazi wasiwaruhusu watoto wao kwenda shule kuanzia leo.

Wanafunzi 180 kutoka Pemba, walifukuzwa KTC walipoandamana kupinga kukataliwa kuandikishwa kupiga kura katika uchaguzi uliopita. Wizara ya Elimu baadaye iliamuriwa na mahakama kuwarudisha wanafunzi hao wote. Wanafunzi 140 walirudishwa bila ya masharti yoyote lakini 40 kati ya hao walikubaliwa wasome tu katika vyuo vya Unguja lakini wajitafutie wenyewe vyakula na malazi. Mgomo ulioitishwa, ambao umethibitishwa kuwa utaanza leo, na kuhusisha shule zote za maandalizi, msingi, kati na sekondari, ni wa kupinga uamuzi huo wa serikali.

Waziri wa Elimu, Bw. Ramadhani Mapuri, jana alitangaza radioni kupinga mgomo huo na kuilaumu CUF kwa kuandaa mgomo huo. Wale wanafunzi 140 waliorudishwa bila ya masharti, nao wamegoma kurudi chuoni hadi hapo wenzao watakaporudishwa kusoma bila ya masharti.

Inasemekana kuwa hali ya kisiasa Pemba ni mbaya sana na jana askari wa Polisi na FFU walionekana kukizunguka kituo cha Polisi cha Wete (anachoshikiliwa Bw. Ahmed Seif Hamad), huku wakiwa na machela na mabomu ya machozi.

Wakati huo huo, kuna tetesi kuwa walimu 12 wa KTC wanatarajiwa "kuingwa" kufuatia shutuma ya kujihusisha na siasa (CUF) chuoni hapo.

Sauti ya Tanzania Zanzibar, na RTD siku mbili hizi wanatoa mazungumzo baada ya habari yanayowaponda CUF na wafuasi wao kwa kudai ushindi wa Seif Shariff Hamad. Mazungumzo hayo yanadai kuwa Uamuzi wa Tume za Uchaguzi, kwa mujibu wa Katiba, hauwezi kusailiwa na yeyote yule hata Rais wa Jamhuri ya Muungano. Hiyo ni katika kujibu tahadhari ambayo viongozi wa CUF wamekuwa wakimpa Rais Mkapa kuwa aiingilie kati suala hilo kwani kuna hatari ya kuzuka fujo Z'bar.

Yarabi salama!
The letter from whom knows Zanzibar condition well.Oct.29.'95
E-mail from Tanzanian overseas.Oct.30.'95
E-mail from Tanzanian overseas .Nov.15.'95
E-mail from Anonymous Oct.31-Nov.3
E-mail from Tanzanian overseas Nov.19.'95
E-mail from Anonymous Nov.25
E-mail from Anonymous Nov.26
E-mail from Anonymous Dec.23
E-mail from Anonymous Jan.29
Zanzibar election Diary19-27 Oct.95
back to Home page